kotii

kotii

HITAJI LA MOYO SEHEMU YAA KWANZA

RIWAYA:HITAJI LA MOYO
MWANDISHI/MTUNZI :Gaooh Mussah
Whatsapp 0654387935

             Kisa cha kwanza Usaliti 1
Hitaji la mwanadamu ni kuishi kwa furaha, furaha iliyomezwa na amani ya moyo. Furaha ya maisha itakayoziba machungu na maumivu hasa kwa kila mwanadamu. Naamini kila mmoja hupenda furaha si furaha ya usoni laa hasha! bali furaha ya moyo itakayomwacha na tabasamu pana kila wakati na kumsahaulisha maumivu ya maisha na mapenzi.
Mbali na maumivu yale ya penzi lakini hayakumbadilisha, jambo hisia liliteka nafasi kubwa ya moyo wake pasi na kumpa nafasi ya kuruhusu mawazo kumbadilisha.
Hakika moyo wa kupenda hauna mtetezi. Hupendelea kusimama pale unapopenda. Moyo umejaa uvumilivu usio na kigeugeu cha kubadili maamuzi kwa muda mfupi. Moyo ni rafiki mwema kwa mwanadamu tofauti na nafsi iliyoumbwa kwa tamaa za kutamani visivyo vyake kiasi cha kujiumbia maumivu ambayo huenda yanaweza epukika.
Nafsi inashindwa  kuiga mfano wa moyo na kufanya vile itakavyo. Mwisho wa siku nafsi inaishia kujisuta yenyewe na kukosa wapambe wa kuipaka majivu.
Ukubwa wa jina la shule  na sifa zake kutokana na kuanzishwa kwake muda mrefu kiasi cha kubeba historia  ya wilaya, ndiyo ilikuwa kitambulisho pekee cha kuitambulisha shule ile ya kata, mbali na ufaulishaji wake kwa wanafunzi hasa baada ya mitihani wanafunzi wengi kupata alama nzuri za kujiendeleza na elimu za juu.
Naam! Iliitwa Mazinde Day Secondary School, jina ambalo lilipatikana kutokana na jina la kata hiyo kwa vile ni shule ya kwanza kuanzishwa katika kata hiyo ambayo iliitwa Mazinde inayopatikana katika mgawanyo wa wilaya mbili za Korogwe nikimaanisha Korogwe mjini na Korogwe vijijini. Kata hiyo ya Mazinde ilifunikwa na mwamvuli wa Korogwe vijijini huku tarafa yake ikiwa ni Mombo.
Shule hiyo ilipata kuanzishwa mwaka 1995 baada ya kuwa hospitali ya wajerumani ndipo ilibadilishwa na kuwa shule. Shule ya sekondari ikiwa katikati ya mashamba ya mkonge.
Sifa za shule hiyo kutokana na ufaulishaji wake na sifa nyingine mbali mbali, ndiyo ilikuwa silaha kubwa ya kujizolea wanafunzi wengi, tena wengine wakitoka mbali na mkoa wa Tanga.
Binti aliyetambulika kwa jina la Na­tasha alikuwa miongoni mwao hasa akitokea mkoa mwengine tofauti na Tanga,
Alitokea mkoa wa Morogoro jiji kasoro bahari, alikozaliwa msanii mkubwa wa Bongo fleva Belle 9 hutakosea ukimwita Belle tisa au jina lake halisi Abelnego.
Natasha alipendeza kwa muonekano wake, hasa akibeba umbo lisilo na ubaguzi wa nguo. Kila nguo ilimkaa na kumpendeza.
Haikuishia hapo alipewa rangi halisi ya mtan­zania nikimaanisha nyeusi, huku mdomoni meno yake yakiacha mwanya mdogo ulioyapendezesha. Alipewa zawadi ya macho yaliyojaa hamasa ya kuangaliwa kila mara, kiasi cha kufanya wamtazamao wasichoke  kutazamana naye.
Haikuishia hapo,umbo namba nane kama sio saba lilimpendeza vyema. Guu la bia na hipsi za haja hazikuacha kuonesha uwepo wake kwenye mwili wa Natasha.
Natasha alijiunga na shule hiyo akianzia kidato cha kwanza. Alikaa katika mabweni ambayo hayakuwa rasmi, kwavile shule hiyo serikalini ilitambulika kuwa ni shule ya kutwa hivyo hata mabweni yake hayakuwa mengi zaidi ya majengo mawili tu tena yakiwa ya jinsia ya kike pekee. Wavulana hawakuwa na nafasi ya kuishi ndani yake.
Uzuri wa Natasha sambamba na heshima na adabu pamoja na upole vilikuwa kivutio kikubwa  kwa wanafunzi wenzake kiasi cha kumpenda. Hakuwa mbaguzi. Aliwajali wanawake kwa wanaume. Alikuwa na tabia njema ambazo zilikuwa ni mfano wa kuigwa na wengine.
Mbali na uzuri aliokuwa nao mpaka kufikia wakati huo akiwa kidato cha kwanza hakuwa akimjua mwanaume yeyote. Hapa ninamaanisha alikuwa hajaijua safari ile ya mapenzi, japo aliwahi kusumbuliwa na wanaume kadhaa huko Morogoro akiwa masomoni lakini hakuwakubali.
Kutokuwa na mpenzi ndio lilikuwa jambo bora lililomkusanyia marafiki wa kutosha. idadi ya marafiki zake ilimezwa na wingi wa marafiki wa kiume japo alikuwa na marafiki hao lakini haikumfanya aingie katika vishawishi nao.
Alikijali kilichompeleka shuleni ambacho ni masomo pekee. Hakuwa na muda wa kusikiliza maneno yoyote yasiomfaa. Hiyo ikawa silaha kubwa ya kuwakata vilimi wale waliokuwa na tamaa naye.
Japo uzuri wake ulimfanya apitie vishawishi vingi kwa wanaume, lakini haikumbadilisha msimamo wake alioushikilia. Vile vile hakutaka kuwa na mpenzi kwa wakati huo .
Maisha ya shule nayo yaliendelea huku siku nazo zikiteketea. Siku hizi zilifanikiwa kumbadili badala ya kuwa mgeni sasa alikuwa mwenyeji wa shule hiyo.
Alipendwa na kila rika hata walimu walivutiwa naye kwa tabia yake ya kuwajali wengine. Looh! Hakujua kijacho mbele yake.
Natasha John alivutika na ushawishi wa kijana aliyeitwa Hudson Aidan. Kijana huyu alimzidi kidato kimoja. Natasha akiwa kidato cha pili na Hudson akiwa kidato cha tatu.
Looh! Hakujua ya ndani ya  kijana yule. Furaha pekee ilikuwa kupendwa naye akiamini amepata wa kumpenda tena aki­jiona kachelewa kupendwa nae. Hakika usilolijua sawa na usiku uliojaa giza.
Hudson alimwumiza Natasha kwa kumsaliti. Kisingizio ni kukosa penzi kwake.
Hilo lilimuuma sana Natasha. Msimamo aliyojiwekea wa kutojishughulisha na mapenzi mpaka aingie kwenye ndoa ndio yalikuwa malipo yake.
Ndugu msomaji penzi ni msumali ugongao mahali pasipostahili kugongwa. Natasha alitupa jiwe sokoni.
ITAENDELEAA.

Burudika nasi, na ujifunze nasi

No comments

'; (function() { var dsq = document.createElement('script'); dsq.type = 'text/javascript'; dsq.async = true; dsq.src = '//' + disqus_shortname + '.disqus.com/embed.js'; (document.getElementsByTagName('head')[0] || document.getElementsByTagName('body')[0]).appendChild(dsq); })();